TOFAUTI KATI YA WANAZUONI (INTELLECTUALS) NA WASOMI (INTELLECTS)


TOFAUTI KATI YA WANAZUONI (INTELLECTUALS) NA WASOMI (INTELLECTS)

Mwanazuoni ni nani? Je, kuna tofauti kati ya mwanazuoni (intellectual) na msomi (intellect worker/intelligentsia)?

 

Ndiyo, ipo tofauti. Wanazuoni wote, au karibu wote, ni wasomi lakini siyo wasomi wote wanakuwa wanazuoni. Mara moja moja inatokea kwamba mtu ambaye hajawahi kusoma katika taasisi yeyote ya elimu huwa mpevu kifikra na kwa hiyo huwa na sifa za mwanazuoni. Lakini hii ni nadra sana. Kwa kawaida wanazuoni wengi huwa wasomi. Kwa hivyo, hatuna budi tuanze kwa kueleza wasomi ni nani.

 

Msomi huishi kwa nguvu-akili wakati mvujajasho huishi kwa nguvu-mwili. Kwa maneno mengine, mfanyakazi huishi kwa jasho lake lakini msomi huishi kwa ubongo wake. Katika mfumo wa kibepari hii ni aina mojawapo ya mgawanyo wa kazi. Na tofauti kati ya msomi na mfanyakazi ni kubwa na ya kipekee. Inakuzwa, inatuzwa.

 

Msomi hujivunia utaalamu na uelewa wake. Na kusema ukweli wasomi wanakubalika katika jamii kama wanataaluma ingawa utaalamu wao unaweza ukawa mkubwa juu ya jambo dogo. Elimu ya kibwanyenye huigawanya taaluma katika visehemu vidogo vidogo. Kwa hivyo, kwa mfano, msomi wa uchumi siyo mtaalamu wa uchumi kwa ujumla, bali anaweza akawa mtaalamu wa fedha tu au wa sarafu tu na asiwe na ufahamu wowote wa uchumi kwa ujumla.

 

Msomi wa sheria anaweza akawa mtaalamu wa masoko ya hisa tu. Anawashauri wacheza “kamari” katika soko hili - ni wakati gani mwafaka wa kununua hisa na wakati gani wa kuziuza ili kujiongezea faida na utajiri. Mfano mmojawapo wa mtaalamu wa masoko ya hisa na fedha ni George Sorros, anajulikana kama msomi aliyejitajirisha kwa kuhamishahamisha fedha kutoka soko moja kwenda soko jingine. Baada ya kutengeneza faida na kutajirika kwa njia hii sasa anafadhili mashirika yasiyo ya kiserikali ya kutetea mfumo wa demokrasia ya kiliberali katika nchi nyingi, pamoja na Afrika.

 

Huyu ni msomi; anachuma fedha na kuishi maisha ya anasa na ya heshima kwa kutumia akili zake “shupavu” za kucheza “kamari”. Wako wasomi wa aina nyingi tu – wakuu wa mashirika ya biashara, wahandisi, wanasheria, wanasiasa, wanaharakati, wahadhiri, watumishi wa ngazi ya juu katika serikali, biashara, viwanda na wengine wengi. Lakini wengi hawa siyo wanazuoni. Wanazuoni hutofautishwa na wasomi kwa sifa kama sita hivi.

 

Moja ni kwamba mwanazuoni huchambua mambo kihistoria. Tukio au jambo limetoka wapi, liko wapi na linaelekea wapi. Mwongozo wake ni kuchambua mielekeo. Tukifananisha na mpiga picha, tunaweza kusema kwamba mwanazuoni hupiga video, sio picha. Hii haina maana kwamba kila mwanazuoni ni mwanahistoria. La hasha! Haiwezekani. Lakini kila mwanazuoni ana mwelekeo wa kihistoria katika uchambuzi wake.

 

Pili, na hili lina uhusiano wa karibu na hilo la kwanza, ni kwamba anaangalia mambo – hususan ya kijamii – katika uhusiano wake na mambo mengine. Kwa mwanazuoni, hakuna jambo lisiloingiliana na jingine. Kuweza kuelewa mwingiliano ni muhimu, badala ya kulitenganisha tukio au jambo na muktadha wake. Kwa mfano, huwezi kuelewa chanzo au vyanzo vya umaskini katika jamii bila kuelewa historia yake na uhusiano wake na utajiri. Umaskini na utajiri ni kama mapacha na vina historia moja. Matajiri wachache wananeemeka na umaskini wa wengi. Kwa hivyo, kuna mwingiliano kati ya umaskini na utajiri. Hata hivyo, baadhi ya wasomi huchambua umaskini bila kuangalia historia yake na kuchukulia, bila kudadisi, kana kwamba umaskini umekuwepo tangu enzi za kale na utaendelea kuwepo milele, isipokuwa labda unaweza kupunguzwa. Tuna mashirika mengi yanayozungumzia upunguzwaji wa umaskini (poverty alleviation) badala ya utokomezaji wa umaskini. Na huwezi kutokomeza umaskini bila kuelewa vizuri chanzo cha umaskini, uhusiano wake na utajiri na mfumo wenyewe unaozaa matabaka ya walionacho na wasionacho.

 

Tatu, mwanazuoni huamini kwamba ukweli haugawanyiki, the truth is the whole. Maana yake ni kwamba huwezi kupata ukweli wa jambo kama hujaliangalia jambo hilo katika muktadha wake. Nikitoa ule mfano maarufu, huwezi ukasema kwamba tembo ni kama kamba nene kwa sababu umegusa mkia wake au kwamba tembo ni mpana kwa sababu umegusa sikio lake. Ili kujua ukweli wa umbo la tembo ni lazima uangalie umbo lake zima. Nitoe mfano mwingine. Ukitaka kuchambua muundo wa kiti, huwezi ukachambua miguu yake tu. Wala huwezi kusema kwamba sehemu za kiti ni miguu na sehemu za kukalia na kuegemea. Ukijumlisha sehemu hizo hutapata kiti, utakachopata ni rundo la mbao! Ukitaka kuelewa muundo wa kiti kizima, huna budi uchambue jinsi na katika uhusiano upi, sehemu zake zote zimeunganishwa.

 

 Nne, mwanazuoni ni wakala wa mabadiliko ya hali iliyopo, na siyo mtumwa wake. Dhamira yake ni kuigeuza na siyo kuigandisha hali iliyopo. Dhamira yake ni kuleta hali bora katika jamii, hususan kwa walio wengi. Yeye daima ni mpambanaji. Anapambana dhidi ya dhuluma, uonevu, ukandamizaji na uovu mwingine popote pale ulipo. Ndiyo dhamira yake, ndiyo maisha yake, ndiyo uhai wake. Anajitambulisha na wapambanaji wenzake bila kujali wanakotoka, makabila yao, au rangi yao. Jamaa mmoja alimwandikia Che Guevara kwamba kutokana na majina yao kufanana labda wao ni ndugu wa damu. Che alimjibu kwamba yeye haoni kwamba wao ni ndugu: ‘Lakini’, namnukuu, ‘kama wewe unachukia uonevu popote pale ulipo, basi sisi ni ndugu, makamaradi …. bila kujali kama sisi ni ndugu wa damu’.

 

Tano, mwanazuoni hujali na kupigania maendeleo ya wanadamu, maendeleo ya wote, siyo ya wachache. Sita, ili kukidhi uelewa wa jamii na mazingira yake na ya ulimwengu, mwanazuoni hujikita kwenye uchambuzi wa kina, uchambuzi ambao unaongozwa na nadharia iliyopevuka. Ndiyo maana wanazuoni wengi, hususan wa Afrika, wanavutiwa zaidi na nadharia ya kimapinduzi ya usoshalisti. Kwa mwanazuoni huyo, ufahamu/elimu ni zana ya kukosoa hali ilivyo bila kusita na kuielekeza kwenye kubadili jamii, siyo bidhaa ya kuuzwa. Katika kusisitiza umuhimu wa nadharia ya kimapinduzi Amilcar Cabral, mkombozi na kiongozi wa Guinea Bissau, alisema: ‘Bila nadharia ya kimapinduzi hakuna mapinduzi yatakayoshinda’. Ni wazi kwamba sio kila mwanazuoni ana sifa hizo zote kama itaeleweka vizuri zaidi katika sehemu inayofuata kuhusu wanazuoni na matabaka ya kijamii. Wanazuoni wa tabaka Wanazuoni ni sehemu ya jamii na wana uhusiano na jamii. Hawawezi kudai kwamba wao ni wachambuzi tu wa mambo na kwamba taaluma yao haiguswi kwa namna yoyote ile na matakwa, hofu, hisia, matumaini, fikra, itikadi na mitazamo ya jamii. Kwa kuwa jamii yenyewe ya kibepari imegawanyika katika matabaka na makundi basi wanazuoni pia huwa wasemaji wa tabaka fulani au kundi fulani, ama bila kujua au bila ya kujitangaza.

 

Tabaka linalotawala hutawala pia mawazo, fikra na itikadi, ndiyo maana katika mfumo wa kibepari itikadi ya kibwanyenye hutawala. Wanazuoni na wasomi wengi hutumikia tabaka-tawala kwa njia moja au nyingine kwa kujenga na kusambaza itikadi yao. Hata hivyo, wanazuoni wachache hutamani kujiunga na wanyonge na kuwatetea. Hao ndiyo wanazuoni wa kimapinduzi. Hakuna mwanazuoni au msomi asiyejikita ama kwenye tabaka-nyonyaji au tabaka-nyonywaji. Wote hujikita kwenye tabaka fulani hata kama hawajitambui au kujitambulisha hivyo. Na mara nyingi, unaoonekana kama mgongano wa kimawazo au kinadharia ni mgongano wa mtazamo uliojikita kwenye tabaka au kundi fulani.

 

Mwanazuoni hufanya uchambuzi wa kijamii ili ayaelewe vizuri mazingira kwa shabaha mahsusi ya kuboresha hali ya maisha ya walio wengi. Yeye huanika uovu wote hadharani bila kujipendekeza. Katika hili uchambuzi wake unakuwa kamilifu bila kujali utamfurahisha nani na utamuudhi nani, na hata kama akisakamwa na wenye mamlaka na madaraka katika jamii, - wakiwemo watawala wa kisiasa au watawala watarajiwa au watawala wa kiuchumi, - hasiti kusema ukweli kama uchambuzi wake unamuelekeza kufanya hivyo.

 

 Kwa vyovyote vile, mwanazuoni mwanamapinduzi hawezi kukosa kuchukiwa na watawala na wenzao wa tabaka la kisiasa, political class. Kama mwanafalsafa wa kimapinduzi Karl Marx alivyosema: “It is certainly not our task to build up the future in advance and to settle all problems for all time, but it is just as certainly our task to criticise the existing world as ruthlessly in the sense that we must not be afraid of our own conclusions and equally unafraid of coming into conflict with the prevailing powers.” Kwa muhtasari, anachosema Marx ni kwamba kwa hakika siyo kazi ya wachambuzi au wanafalsafa kutanguliza kujenga mustakabali na kutatua matatizo yote kwa enzi zote, lakini ni kwa hakika pia kazi yao ni kukosoa hali ya ulimwengu iliyopo wakati huo bila kusita na kutokuhofia matokeo ya uchambuzi wao hata kama haya yatawaingiza kwenye misuguano na wenye madaraka.

 

Niongeze kusema kwamba ni wazi kabisa kwamba wanazuoni wanaotetea hali ilivyo bila shaka hawatakabiliwa na upinzani mkubwa kutoka kwa wale wanaofaidika na hali hiyo. Kwa upande mwingine, wale wanaotaka kubadili hali kwa mtazamo wa wavujajasho watakuwa na hali ngumu, watasakamwa, watatungiwa uongo, watadhalilishwa na hata kujeruhiwa au kuuawa. Kwao hii siyo hoja. Katika misitu ya Bolivia, wakati Che Guevara alipokutana ana kwa ana na wanajeshi mamluki wa Serikali, mmoja wao alimtambua na kulenga bastola yake kwake. Lakini alikuwa anasitasita kuifyatua. Che akamwambia, kwa sauti ya utulivu; ‘Unasita nini. Fyatua risasi yako, utakuwa umemuua mtu tu!’, kwa maana kwamba huwezi kuua fikra na mtazamo wa mwanamapinduzi na kweli kabisa mpaka leo fikra za Che zimedumu.

 

Katika historia yetu ya mapambano ya ukombozi tuna mifano mingi ya wanazuoni waliojitolea mhanga kwa sababu ya msimamo wao kuwa upande wa umma. Patrice Lumumba alitaka nchi yake iwe na uhuru kamili ili iweze kutumia utajiri wake kwa manufaa ya, siyo Wakongomani tu, bali kwa manufaa ya watu wa Afrika kwa sababu Lumumba alikuwa muumini wa Umajumui wa Afrika (Pan-Africanism). Aliuawa kikatili na wakala wa CIA.

 

Kwame Nkrumah wa Ghana aliuchambua na kuukusoa mfumo wa ukandamizaji wa kibeberu, akitaka kuleta Umoja wa Afrika kwa sababu aliamini kabisa kwamba wananchi wa vinchi vya Afrika wakiwa peke yao, hawataweza kumudu nguvu za kibeberu. Akapinduliwa na waliochukua madaraka kama mwanajeshi Afrika aliyekuwa na mawazo finyu, wakamsakama na kumdhalilisha. Chris Hani, ambaye alikuwa na dhamira ya kujenga Afrika Kusini mpya kwa mtazamo wa wavujajasho, aliuawa katika kipindi nyeti cha mpito kutoka ukaburu kwenda ukombozi. John Garang, kiongozi wa muda mrefu wa Sudan Kusini, alikuwa na msimamo wa kutokutenga na kuvunja nchi ya Sudan, badala yake alitaka Sudan Mpya. Umma wa Sudan Kusini na Sudan Kaskazini walikuwa nyuma yake. Inasemekana alikufa katika ajali ya helikopta. Sina hakika!

 

Muammar Gadaffi, mwanasiasa aliyekuwa na dhamira ya kuleta mabadiliko makubwa na yenye maslahi kwa nchi na jamii yake, ingawa baadaye alianza kuyumbayumba, aliuawa na majeshi ya mamluki yakisaidiwa na NATO. Kosa lake? Alikuwa na mpango kabambe wa kuvuna maji yaliyopo chini ya ardhi ya jangwa la Sahara na kueneza maji hayo katika eneo lote la Sahel. Lakini Rais wa Ufaransa, wakati ule Sarkozy, alikuwa na mpango wake mbadala. Alitaka Gadaffi akubali kutoa idhini ili mashirika ya Kifaransa wayavune maji hayo na kuyasafirisha kwenda Ufaransa kwa ajili ya kutengeneza maji ya chupa. Gadaffi alikataa katakata. Akasukiwa mpango, nchi yake ikavamiwa na hatimaye akauawa. Leo hii nchi ya Libya imesambaratishwa na hao hao waliojiita wakombozi. Nchi na vyombo vya habari vya Magharibi waliwakuza sana vibaraka hao na kuwatambua kama “wakombozi”, ili kuhalalisha maslahi yao ambayo yalikuwa sababu kuu ya kumpindua na kumuua Gadaffi.

BY ISSA SHIVI

GAZETI LA RAIMWEMA TOLEO NAMBA 351

MAY 7, 2014

1 comment: